Ilikuwa miaka, miezi, wiki, siku na sasa ni saa tu kwa mambo kuwa
hadharani nchini Brazil katika ufunguzi wa michuano ya Kombe la Dunia.
Katika taifa hilo la wachawi wa soka na samba, Brazil wanaanza kwa kucheza na Croatia usiku wa Alhamisi hii.
Brazil wanatarajiwa kuingiza dimbani kikosi kile kile kilichowanyoa Wahispania kwenye fainali ya michezo ya Kombe la Mabara.
Kiungo mchezeshaji, Oscar, anatarajiwa kuanza licha ya kutokuwa
katika kiwango cha hali ya juu huku vyombo vya habari vikimpigia debe
mchezaji mwenzake wa Chelsea, Willian.
Croatia wanaanza bila mpachika mabao, Mario Mandzukic anayetumikia
adhabu ya kukosa mechi moja, hivyo Nikica Jelavic au Eduardo watashika
nafasi yake.
Sime Vrsaljko atacheza katika beki ya kushoto badala ya majeruhi Danijel Pranjic
Sherehe za ufunguzi zinakuja baada ya mechi 820 za kufuzu
zilizoshirikisha timu 202 kutoka mabara yote na kuchujwa hadi kufikia
timu 32 tu zilizoingia kwenye fainali hizi.
Hizi ni fainali ambazo ni za gharama kubwa zaidi katika historia ya
Kombe la Dunia na baadhi ya wananchi wa Brazil waliandamana kupinga
matumizi hayo, wakidai kwamba bora fedha zingeelekezwa kuboresha maisha
yao, jambo ambalo limebezwa na wananchi wengi pamoja na viongozi wao.
Mchezo wa usiku huu unakuja wakati ambapo historia ikionesha hakuna
nchi mwenyeji iliyopata kupoteza mechi ya ufunguzi, hivyo shinikizo lipo
kwa Brazil.
Kocha wa Vroatia, Niko Kovac amesema kwa kuwa wakweli ni kwamba
Brazil wanapewa nafasi ya kushinda mechi hiyo kutokana na uenyeji lakini
pia kwa uwezo wa wachezaji wake wenye vipaji.
“Tumekuja kwa ajili ya kucheza, kushindana na tutaonesha uwezo wetu
wote uwanjani. Wachezaji wana ari kubwa kwa mechi hii inayosubiriwa na
mamilioni ya watu kote duniani. Wataonesha kiwango cha hali ya juu,”
anasema Kovac.
Mechi ya mwisho iliyokutanisha timu hizi ilifanyika 2006 ambapo
Brazil walishinda 1-0 kutokana na bao la Kaka jijini Berlin, Ujerumani.
Agosti 2005 timu hizo zilitoka sare 1-1 katika mashindano mengine, na nchi hizi hazijakutana tena.
Brazil wameshinda mechi zao tisa zilizopita wakifunga mabao 30 na
kufungwa mawili tu, hivyo kuonesha jinsi walivyo na uwezo mkubwa.
Wamefungwa mechi moja tu kati ya 21 zilizopita.
Brazil ni nchi pekee ambayo haijakosa hata fainali moja ya Kombe la Dunia tangu kuanzishwa kwake.
Katika mashindano hayo wameshinda mechi 67, wakafunga mabao 210
lakini ni wachezaji sita tu katika kikosi cha sasa ambao wamepata
kushiriki michuano hii, ambapo wanafundishwa na Luiz Felipe Scolari ‘Big
Phil’ ambaye ni Mbrazili.
Tangu Kovac awe kocha wa Croatia, hawajafungwa katika emchi tano ambapo wameshinda tatu na kwenda sare mbili.